12/06/2026
DODOMA.
Huzuni na majonzi vimetawala katika Chuo Kikuu cha St. John, jijini Dodoma Leo 12 juni 2026,wakati wa ibada ya kuaga mwili wa mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa fani ya Afya, Rebeca James Misungwi, aliyefariki dunia baada ya kujeruhiwa katika ajali ya moto iliyotokea usiku wa kuamkia Jumapili, Juni 7, 2026, katika nyumba aliyokuwa akiishi pamoja na rafiki yake, Felister Peter Francis ambaye anaendelea na matibabu Katika hospitali ya Benjamini Mkapa.
Rebeca alifariki dunia Juni 11, 2026, katika Hospitali ya Benjamin Mkapa alipokuwa akipatiwa matibabu kutokana na majeraha aliyoyapata kwenye tukio hilo. Baada ya ibada ya kuuaga mwili wake iliyofanyika chuoni hapo, mwili umesafirishwa kuelekea mkoani Mwanza kwa ajili ya mazishi.
Akizungumza kwa niaba ya familia, kaka wa marehemu, Pascal Kapote, amesema wamepokea kwa masikitiko makubwa msiba huo na kuliomba Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha tukio hilo na kuhakikisha mtuhumiwa anayehusishwa na tukio hilo anachukuliwa hatua za kisheria.
"Familia inaamini kuwa haki itatendeka kupitia uchunguzi wa vyombo husika," amesema Pascal.
Aidha, amesema baada ya kuuaga mwili huo, familia inaelekea mkoani Mwanza kwa ajili ya maandalizi ya mazishi, huku akibainisha kuwa ratiba kamili ya mazishi itatangazwa mara baada ya mwili kuwasili nyumbani.
Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo ili kubaini mazingira halisi yaliyosababisha ajali hiyo ya moto.