13/08/2026
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Dodoma limetoa elimu ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa vitendo kwa maafisa wa Jeshi la Polisi ngazi ya kata, wilaya na mkoa, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati hiyo katika shughuli za kila siku.
Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Mkoa wa Dodoma, James Vesso, amesema wameona umuhimu wa kutoa elimu hiyo kwa vitendo ili kuwawezesha maafisa hao kuwa mabalozi wa nishati safi ya kupikia na kuwafikishia elimu hiyo wenzao pamoja na jamii kwa ujumla.
Vesso amesema matumizi ya majiko ya umeme ni miongoni mwa njia salama na nafuu za kupikia, huku yakitumia muda mfupi ikilinganishwa na baadhi ya njia nyingine za kupikia. Amesema ongezeko la watumiaji wa majiko ya umeme linaendelea kuonekana kutokana na elimu inayotolewa pamoja na ushirikiano wa TANESCO na wadau katika kuwawezesha wananchi kupata majiko hayo.
Ameeleza kuwa TANESCO na wadau wake wamekuwa wakiwezesha wananchi kupata majiko ya umeme kwa mikopo yenye masharti nafuu, ambapo mteja hupewa fursa ya kuchagua utaratibu unaomfaa wa kufanya malipo. Miongoni mwa njia hizo ni malipo kupitia mfumo wa LUKU, ambapo kiasi cha malipo hukatwa kidogo kidogo wakati mteja anaponunua umeme, pamoja na utaratibu mwingine wa kulipa kwa awamu.
Elimu hiyo imetolewa wakati TANESCO Mkoa wa Dodoma ikiendesha kikao kazi maalum na viongozi wa Jeshi la Polisi ngazi ya kata, wilaya na mkoa,Leo 13 August 2026 ambapo pamoja na masuala ya nishati safi, pande hizo zimeweka mikakati ya pamoja ya kuimarisha ulinzi wa miundombinu ya umeme mkoani Dodoma.