27/02/2026
TUPATE KUJIFUNZA KIDOGO JUU YA "BARAKA" ZA MUNGU.
BARAKA SI BIASHARA
●Ndugu zangu, ni wakati wa kuamka kiroho. Kuna wimbi la mafundisho yanayowafanya waamini kuwa baraka na ulinzi vinaweza kuuzwa k**a bidhaa. Wengine wanaambiwa watoe kiasi fulani ili wapate “ufunguzi,” “kinga maalum,” au “neema ya kasi.” Hii ni hatari kwa sababu inageuza imani kuwa biashara na madhabahu kuwa soko.
●Maandiko yanasema wazi katika Isaya 55:1, “Njoni, nunueni bila fedha na bila thamani.” Hii inaonyesha kwamba neema ya Mungu haitolewi kwa bei ya pesa. Mungu hatoi baraka kwa sababu ya kiasi ulichotoa, bali kwa sababu ya neema yake na uhusiano wako naye. Pale fedha zinapokuwa sharti la kupokea ulinzi au baraka, tayari tumepotoka.
●Katika Matendo ya Mitume 8:18-20, Simoni alipotaka kununua kipawa cha Mungu, alikemewa vikali. Aliambiwa wazi kuwa moyo wake haukuwa sawa mbele za Mungu. Hii ni fundisho kubwa: mambo ya kiroho hayawezi kununuliwa. Yananunuliwa kwa toba, imani na utii—si kwa noti za pesa.
●Ulinzi wa kweli unatoka kwa Mungu, si kwa mtu. Zaburi 121:7-8 inasema, “Bwana atakulinda na mabaya yote; atailinda nafsi yako.” Hakuna mtumishi aliye chanzo cha ulinzi wako; yeye anaweza kukuombea, kukushauri na kukufundisha, lakini mlinzi wako ni Mungu mwenyewe. Kumfanya mtumishi awe chanzo cha kinga ni kumweka mahali pa Mungu.
☆Onyo ni hili: ukifundishwa kuwa bila kulipa huwezi kulindwa au kubarikiwa, fahamu kwamba unafungwa kwa hofu. Injili ya kweli haijengwi juu ya hofu, bali juu ya upendo na neema. Mungu halazimishi; anaita. Mchungaji au mtumishi wa kweli hatishii waumini ili watoe, bali hufundisha ukweli kwa uwazi.
♤Hii haimaanishi kuwa utoaji si wa muhimu. Utoaji ni sehemu ya ibada na shukrani. Lakini utoaji wa kibiblia hutoka moyoni, si kwa masharti ya kupata “kinga maalum.” Ukitoa kwa hofu au kwa kulazimishwa, tayari umepoteza maana ya sadaka.
=>>Ushauri wangu kwa Wakristo ni huu: someni Neno la Mungu wenyewe. Msijenge imani juu ya maneno ya mtu pekee bila kuyachunguza katika Maandiko. Mkijua ukweli, hamtapotoshwa kirahisi. Ukweli huweka huru; ujinga huweka kifungoni.
•Pia waheshimuni watumishi wa Mungu wa kweli, lakini msiwaabudu. Heshima ni ya kibiblia, lakini ibada ni ya Mungu pekee. Mtumishi ni chombo, si chanzo. Akianza kujiweka k**a chanzo cha baraka au ulinzi, hapo panahitaji tahadhari ya kiroho.
▪︎Lengo si kushambulia watu, bali kurejesha kanisa kwenye msingi wa Injili ya neema. Baraka haziuzwi. Ulinzi haukodishwi. Neema haitangazwi kwa bei. Mungu ni Baba, si mfanyabiashara.
》》》Apostle :Paul N Utta