26/06/2026
Nyota wa soka wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta ameibuka na ujumbe wa kugusa hisia baada ya kuchapisha video inayoonesha maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Kulelea Watoto wenye Uhitaji Maalum ‘Samatta Orphanage Center’.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, leo Juni 25, 2026 Samatta ambaye kwa sasa anakipiga katika klabu ya Le Havre AC ya Ufaransa (Ligue 1), amesema mradi huo umekaribia kukamilika na kwamba umepitia changamoto nyingi kabla ya kufikia hatua ya mwisho.
Ameandika kwamba safari ya ujenzi huo imejaa uvumilivu, mapambano na imani, lakini upendo kwa Watoto wenye uhitaji umekuwa chanzo kikuu cha nguvu ya kuendeleza mradi huo.
Akirejea mafundisho ya dini, Samatta amenukuu maandiko matakatifu akisema: “Waacheni Watoto wadogo waje kwangu” (Mathayo 19:14) na pia “Kuwafanyia mema mayatima ndiyo bora” (Qur’an 2:220), akisisitiza umuhimu wa kusaidia Watoto wenye uhitaji.
Ameongeza kuwa Kituo hicho kitatoa mazingira salama, malezi bora, upendo na fursa kwa Watoto hao kutimiza ndoto zao, akisisitiza kuwa ni mradi wa moyo wake unaolenga kurejesha kwa jamii kile alichobarikiwa nacho.
Samatta amehitimisha kwa kuwataka watu kushirikiana katika kubadilisha maisha ya Watoto na kujenga taifa lenye matumaini kwa kizazi kijacho.